WANAFUNZI 771 KITETO WALIOFAULU HAWAKURIPOTI SEC

 Mohamed Hamad katika harakati za kupiga picha kikao cha bajeti cha baraza la madiwani Kiteto

Wanafunzi 771 Kiteto waliofaulu hawakuripoti sekondari  

Na. Mohamed Hamad Manyara
Jumla ya wanafunzi 771 waliofaulu kujiunga na Sekondari wilayani Kiteto mkoani Manyara wameshindwa kuripoti sekondari kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo kuolewa pamoja na kukosekana kwa mwamko wa elimu kwa jamii

Katibu tawala wa wilaya ya Kiteto Nicodemus John akizungumza kwenye kikao cha Baraza la madiwani leo (jana) alisema idadi hiyo imetokana na wengi wa wanafunzi hao kuwa na wachumba shuleni na baada ya kumaliza kuolewa

“Idadi hii ni kubwa na wala haivumiliki kuona kiasi hiki kikikosa elimu,naagiza kila Katibu Tarafa awe amewabainisha watoto na kuwafikisha wazazi wao mahakamani mara moja”alisema Nicodemas

Kuhusu agizo la Rais kutaka kujengwa vyumba vitatu vya maabara katika kila Sekondari Katibu huyo alisema muda uliongezwa kukamilisha ujenzi huo na kuwataka kila kiongozi wa jamii awajibike katika nafasi yake

Alisema Kiteto inahitaji viongozi wawajibikaji na sio kupiga midomo kwani agizo hilo la Kiongozi wa Nchi ni sheria na atakaye kaidi sheria zitamthibitikia zikiwemo adhabu ya kifungo, faini ama vyote kwa pamoja kutokana na maamuzi ya Hakimu

Kwa upande wake Kidawa Othman Diwani wa kata ya Matui CHADEMA alishangazwa na baadhi ya kata za jamii ya kifugaji wamasai kama vile Makame,Ndedo, Namelock,na Partimbo kushindwa kutekeleza agizo la Rais wakati wana rasilimali nyingi na za kutosha (mifugo)

“Mbona kwenye zoezi la kuwatoa wakulima mashambani wafugaji na rasilimali zenu mliungana kuchangia madume, kwanini agizo hili la Rais mnalisusia kwa kugoma kuchanga fedha kwaajili ya maabara”alisema Kidawa

Kutokana na agizo hilo kata ya Namelock, Partimbo na Makame zimeshindwa kufikia kiwango stahili cha ujenzi ambapo kwa tarafa ya Makame badala ya kila kata kujenga Sekondari yake wameamua kujenga Sekondari ya Tarafa tofauti na agizo la Rais

Kwa upande wake Bosco Ndunguru Mkurugenzi Mtendaji wa Halamshauri ya Wilaya ya Kiteto alizitaka kata hizo kuongeza jitihada akisema kila kiongozi atawajibika katika nafasi yake muda utakapofika akisisitiza kuwa kinachotakiwa ni maabara tatu kila Sekondari

“Kila mtu aguswe na maendeleo ya kata yake sioni sababu ya suala hili kuonekana kukwama kutokana na kuwepo kwa rasilimali nyingi na za kutosha ndani ya jamii na ikishindikana mabaraza ya kata yatumike kufanikisha zoezi hili”alisema Ndunguru

Mwisho

Maoni