Hatima ya mtoto aliyefia tumboni miaka 5 iliyopita atolewa Kiteto


NA.MOHAMED HAMAD MANYARA
Jopo la madaktari wa hospitali ya wilaya ya Kiteto mkoani Manyara limefanikiwa kuokoa maisha ya Bi.Sinyati Parla (33) kwa upasuaji aliyekaa na mimba ya mtoto wa kiume aliyefia tumboni kwa miaka mitano

Upasuaji huo ulifanyika mwishoni mwa wiki katika hospitali ya Kiteto baada ya mwanamke huyo kulazwa na kufanyiwa uchunguzi na kubainika kuwa alikuwa na uvimbe mkubwa tumboni ambapo alitolewa mtoto wa kiume tumboni akiwa mfu

Akiongea na UWAZI Dr. Leadry Malisa aliyefanya upasuaji huo kwa kushirikiana na Dr Madama Hosea alisema walifanikiwa kutoa maiti hiyo ya mtoto wa kiume iliyokuwa tumboni kwa miaka mitano

“Haikuwa rahisi kama tulivyozoea kufanya upasuaji wa kawaida, lakini kwa mapenzi ya mungu tulifanikiwa na hali ya mgonjwa imeimarika naamini atapona na kuendelea na kazi zake za kawaida za kila siku”alisema Dr Malisa


Hata hivyo jopo hilo la madaktari lilisema kuwa upasuaji huo ulikuwa ni wa aina yake na wakihistoria wilayani humo ambapo wamedai haijapata kutokea toka wilaya hiyo izinduliwe mwaka 1974 kutoa kiumbe mfu kilichokaa kwa miaka mitano tumboni

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili umebaini kuwa mimba hiyo ilikuwa ni ya nne kwa mwanamke huyo ambapo awali alijifungua watoto watatu wote wakiwa salama na afya njema

Katika kuhakikisha kuwa uhai kwa akinamama  wajawazito unaimariishwa Dr Malisa aliwataka wanawake wajawazito kuwa na utamaduni wa kwenda kiliniki mara wanapopata ujauzito kupata ushauri wa kitaalamu hadi watakapojifungua

Akizungumza akiwa amelazwa wodi namba mbili katika Hospitali hiyo mwanamke huyo alitaja baadhi ya Hospitali alizofika kusaka huduma katika kipidi hicho chote kuwa ni pamoja na Seliani ya Arusha, KCMC Moshi na Mhimbili

Alisema alitumia fedha nyingi kusafiri  pamoja na kugharamia za matibabu kwa miaka mitano mfululizo ambapo katika Hospitali ya Kiteto aliitwa tu na ndugu yake aliyempeleka hospitali na kufanyiwa upasuaji huo

“Nawashukuru sana madaktari kwa kazi nzuri waliyofanya kwani sasa nina matumaini mazuri kuisha naamini kuwa nitapona kwa hapa nilipofikia kwani nilishakata tamaa ya kuishi”alisema Bi.Sinyati Parla

Mwisho

Maoni