POLISI YAZIMA VURUGU ZANIBAR,NI BAADA YA MAALIM SHARIF HAMAD KUJITANGAZA MSHINDI WA URAIS


Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad akiongea na wanahabari.
WAKATI wakisubiri matokeo ya uchaguzi ya rais huku Tume ya Uchaguzi ikitangaza kura za wagombea wabunge na uwakilishi katika majimbo ya uchaguzi Zanzibar, Jeshi la Polisi limelazimika kuzima fujo na vurugu kutoka kwa wafuasi wa CUF waliotanda mitaa ya Mji Mkongwe na barabara kuu ya Darajani.
Vurugu zimezuka baada ya mgombea wa Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad kufanya tathmini na kutangaza matokeo ya ushindi wa chama chake katika uchaguzi wa juzi kwa asilimia 52.87. Maalim Seif alitoa tathmini hiyo mbele ya waandishi wa habari katika Ofisi Kuu ya CUF Mtendeni mjini Unguja na kuitaka Tume ya Uchaguzi Zanzibar (ZEC) kutangaza matokeo hayo.
Katika tathmini hiyo inaonesha kwamba mgombea wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kwa tiketi ya urais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein amepata ushindi kwa asilimia 47.13. Maalim Seif alidai matokeo waliyonayo yamekusanywa na mawakala waliopo katika vituo vya uchaguzi vilivyopo Unguja na Pemba kwa kufanya majumuisho. Hatua hiyo ilizusha shangwe na furaha kwa wafuasi wa CUF na kuanza kutembea barabarani huku gari zikipiga honi.
Baadhi ya mitaa ikiwemo Darajani na Mlandege, polisi waliweka vizuizi ambavyo vilisaidia kuwazuia wafuasi hao kuingia barabarani. Aidha, ofisi za Serikali zilizopo katika eneo la Mji Mkongwe pamoja na taasisi za kibenki, zilifungwa baada ya kuibuka kwa mazingira ya fujo na vurugu.
Kamanda wa Polisi mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, Mkadam Khamis Mkadam alithibitisha Jeshi la Polisi kudhibiti maeneo mbalimbali zaidi yaliyopo Mji Mkongwe pamoja na eneo la Darajani ambalo ni ngome ya upinzani.
“Tumefanikiwa kudhibiti vurugu za watu waliofanya fujo na vurugu katika maeneo mbali mbali ya mji wa Unguja na hali ni shwari kwa sasa,” alisema Mkadam. Kwa mujibu wa Sheria na Kanuni za Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ni kosa la jinai kwa mtu yeyote au mgombea wa chama cha siasa kutangaza matokeo ya urais. Mapema, CCM Zanzibar ililaani kitendo kilichofanywa na Maalim Seif kujitangazia ushindi katika uchaguzi huo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar, Vuai Ali Vuai alisema kitendo hicho ni sehemu ya vitendo na matukio ya uchochezi yanayotakiwa kudhibitiwa kwa ajili ya kuimarisha amani na utulivu. Vuai aliitaka ZEC kuchukua hatua za kisheria na kinidhamu kwa mgombea huyo kwa kauli zake ambazo lengo lake kuingiza nchi katika machafuko katika kipindi hiki kigumu cha uchaguzi.
Hata hivyo, viongozi watendaji wa ZEC hawakuwa tayari kulizungumzia suala hilo, ambapo maofisa wote walikuwa wapo katika mchakato wa kupokea na kutangaza matokeo ya uchaguzi wa majimbo.

Maoni