Majaliwa akerwa bidhaa za Tanzania kuwekwa nembo ya Kenya

Waziri Mkuu Majaliwa Kassimu Majaliwa..



Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amekerwa na mifuko ya mbolea ya kiwanda cha Minjingu kuchapishwa anuani ya Kenya wakati inazalishwa Tanzania na kumtaka mwekezaji kumuomba radhi Rais.

Kutokana na hilo, Waziri Mkuu amewataka wamiliki wa kiwanda hicho, waandike barua kwa Rais John Magufuli kabla hajamaliza ziara yake keshokutwa na apate nakala ya barua hiyo.

Alitoa agizo hilo baada ya kutembelea kiwanda hicho kilichopo wilaya ya Babati akiwa katika siku ya tatu ya ziara yake mkoani Manyara. Waziri Mkuu amerejea Babati jana akitokea Dar es Salaam ambako alikuwa na ratiba za kitaifa.

“Nilikuja kukagua kiwanda baada ya kupokea malalamiko kuwa mbolea hii haikubaliki huko vijijini. Watafiti wameonyesha kuwa ikitumika inasaidia kutoa mazao mengi. Lakini wakati niko kiwandani nimekerwa kukuta mifuko ya kupakia mbolea hii ina anuani ya Nairobi, Kenya wakati mali ghafi inatoka Tanzania,” alisema.

“Ni kwa nini mifuko hii ina anuani ya Kenya? Hapa tulipaswa tuone anuani ya Babati! Je mlipata kibali kutoka serikalini? Tena kuna lebo ya TBS. Kwanini Tanzania haionekani? Kwani malighafi iko Kenya? haiwezekani, ni lazima uandike barua na uombe radhi kwa Mheshimiwa Rais Magufuli. Yeye anahimiza ujenzi wa viwanda ndani ya nchi, halafu ninyi mnafanya hivyo?”

Akitoa maelezo kuhusu hali hiyo, Mkurugenzi wa kiwanda hicho, Tosky Hans alimweleza Waziri Mkuu kwamba wametumia lebo hiyo kutokana na makubaliano na wanunuzi jibu ambalo Waziri Mkuu hakulikubali na kusisitiza kuwa anapaswa aombe radhi.

Maoni