DED Kiteto atumbua watumishi wawili

Mkurugenzi Kiteto atumbua mkuu wa idara

Na, MOHAMED HAMAD KITETO.

MKURUGENZI mtendaji wa halmashauri ya Wilaya ya Kiteto, Tamim Kambona, amemsimamisha kazi Afisa mifugo wa wilaya hiyo Bw. William Msuya kwa tuhuma za ubadhirifu wa zaidi ya mil 60.

Fedha hizo ni kwaajili ya gharama ya upigaji chapa ya mifugo wilayani humo, ambapo lengo ni kufikia mifugo 363,128 kati 247,425 iliyopo wilayani humo.

Akizungumza na MTANZANIA, Mkurugenzi Kambona alisema, wakati wa zoezi hilo baadhi ya wafugaji walipewa risiti na wengine kunyimwa kwa maksudi, ulipofanyika ukaguzi walibaini upotevu wa fedha hizo.

Alisema pamoja na kutakiwa kuwasilisha fedha hizo na kikao cha fedha na mipango, Bw Williamu Msuya, alionekana kukaidi na hata kutofika kazini huku akimtuma msaidizi wake kwenye vikao vya kazi.

“Nimempa siku kumi na nne arejeshe fedha hizo mara moja tena aingize benki na kunileteea sleep..hata kwenye vikao anatuma msaidizi, kwa sasa anakuja kazini kwa muda anaotaka, kama hatorejesha mimi nitamfikisha mahakamani”alisema Kambona.

Kambona alisema hatosita kumchukulia hatua mtumishi yoyote atakayeonekana kuihujumu halmashauri, na kutoa onyo kwa watumishi wa idara hiyo ya Kilimo kuwa bado kuna watumishi ambao wameshiriki katika wizi huo kuwa nao wajiandae.

Akizungumzia zoezi hilo, Michael Lepunyati Diwani wa kata ya Namelock alisema, alilazimika kuwa mfano wa kupiga zoezi hilo ili jamii ya kifugaji masai waweze kuiga kwani awali walikataa kwa madai kuwa chapa hiyo inafanya mifugo kutozaa.

“Tumekubaliana wafugaji wote baada ya kutolewa elimu tulianza na kundi la viongozi, tena kwa kuchangia fedha ambazo ni utaratibu wa zoezi hilo ili wafugani waweze kuona kuwa hakuna madhara”, alisema kiongozi huyo.

Mwisho

Maoni