CHADEMA KITETO KUTOSHIRIKI UCHAGUZI MKUU



CHADEMA yatoa siku 10 za kufanya uchaguzi Kiteto.

  • ·         Uongozi wa vijana wavunjwa,waundwa upya.

  • ·         Kutoshiriki uchaguzi mkuu 2015 wasipofuata masharti.

Na. Mohamed Hamad Manyara.
CHAMA cha Demokrasia na maendeleo CHADEMA Taifa kimetoa siku kumi kwa uongozi wa chama hicho Kiteto kufanya uchaguzi ngazi ya chini (Chadema ni msingi) hadi wilaya ili waweze kupata tiketi ya kushiriki uchaguzi mkuu wa 2015.

Mkuu wa itikadi na uenezi Taifa Waitara Mwita akizungumza na kamati ya utendaji wa chama hicho Wilayani Kiteto jana (juzi) alisema ushiriki wa chama hicho uchaguzi mkuu 2015 utategemea kukamilika kwa uchaguzi ngazi ya chini.

“Hatutaivumilia wilaya yoyote ishiriki uchaguzi mkuu mwakani kama hawatafanya uchakuzi ndani ya chama na hili tutalisimamia kikamilifu na wala hatutaona haya kulisemea na mahali popote nchini”alisema Mwita.

Wakati huo kwa mujibu wa katiba ya CHADEMA kiongozi huyo ameufuta uongozi wa vijana wilaya baada ya kuonekana wana  umri mkubwa na kuchaguliwa Abubakari Kidevu kuwa mwenyekiti huku  katibu akiwa Athumani Ismail.

Mbali na hatua hiyo pia kura zililazimika kupigwa kuhusu kuvunja kamati ya utendaji ama kutovunjwa kutokana na kuonekana kushindwa kuwajibika ipasavyo ambapo walilazimika kuongezewa wajumbe wengine ili kusukuma mbele shuhuli za chama.

“Hali haikuwa shwari kwenye kikao, kwani hata kamati ya utendaji ilitakiwa kuvunjwa kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo za kutowajibika ipasavyo hali ilisababisha kudorora kwa chama kipindi chote”alisema Ole Loilole Leng’isya katibu wa Wilaya.

Aidha katibu huyo alisema chama kilitakiwa kufanya uchaguzi huo mwisho june 30 mwaka huu na kwamba kutokana na sababu mbalimbali zilichangia kutofanyika.

Alitaja baadhi ya sababu hizo kuwa ni pamoja na kukosekana kwa amani katika maeneo mengi ya wilaya ya kiteto juu ya migogoro ya ardhi ambayo inaendelea hadi sasa na kusababisha madhara yakiwemo mauaji.

Alisema hali hiyo imekuwa tishio kwa wananchi na hata viongozi wa kisiasa na Serikali kwa ujumla kuendelea kufanya kazi katika mazingira hayo kutokana na kitendo cha mauaji ya kila mara huku kukiwa hakuna jitihada za maksudi kukabiliana na tatizo hilo.

Hata hivyo CHADEMA kwa pamoja wamelaani mauaji yanayoendelea kujitokeza kwa jamii ya wakulima na wafugaji wilayani humo na kuitaka Serikali kuzuia ili kuwapa wananchi waweze kufanya kazi ya ujenzi wa Taifa.

Mwisho.

Maoni