LOWASSA ALIVYOJITETEA JUU YA KILICHOMFANYA ASHINDWE DHIDI YA MAGUFULI


Waziri Mkuu Mstaafu na aliekuwa mgombea urais kupitia Chadema Edward Lowassa akiongea na  wandishi wa habari .Picha na omar fungo
Aliyekuwa mgombea wa urais kupitia Chadema na Ukawa, Edward Lowassa amesema ataendelea kushiriki kikamilifu katika siasa na kubainisha kuwa utaendeleza mapambano ya mabadiliko kwa kudai Katiba Mpya.
Lowassa aliwaambia wanahabari leo kuwa kasi ya ufanyaji wa siasa itaongezeka kuliko ilivyokuwa awali na kwamba kwa sasa anaweza akawa “amepoteza pambano lakini siyo vita.”
Kauli hiyo ya Lowassa inabadilisha msimamo wake wa awali aliokuwa wameutangaza kupitia mahojiano na Shirila la Habari la Uingereza (BBC) kuwa iwapo angeshindwa kinyang’anyiro hicho cha urais angeenda kuchunga ng’ombe kijijini kwake Monduli mkoani Arusha.
Mwanasiasa huyo, ambaye pia ni waziri mkuu wa zamani, alisema Ukawa itaendelea kudai Katiba Mpya ya wananchi itakayohakikisha kuwa Tanzania inakuwa na tume huru ya uchaguzi na serikali inayowajibika kwa umma.
“Ni wazi kuwa uchaguzi mwingine katika mazingira ya sasa na chini ya katiba ya sasa hauwezi kuzaa matunda tofauti. Bila katiba mpya ya wananchi, Tanzania haitakuwa na demokrasia na itaendelea kuwa nchi  inayotawaliwa kwa mizengwe na udikteta wa CCM,” alisema Lowassa.

Maoni