Jamii ya AKIE/WANDOROBO watishia kurudi porini



Jamii ya AKIYEE jina maarufu NDOROBO wanaoishi kwenye maeneo maalumu
yaliyotengwa wilayani Kiteto mkoani Manyara, wameilalamikia Serikali
kushindwa kuwapatia huduma za jamii kama Afya,Elimu,Maji na
Miundombinu

Maeneo wanayoishi jamii hiyo Wilayani Kiteto ni Ngapapa,Leruk  na
Napilukunya, ambapo wamedai awali waliishi maporini bila huduma zozote
za kijamii huku chakula chao kikuu kikiwa mizizi, asali na nyama
Wamesema serikali iliwataka kuishi pamoja katika maeneo hayo kwa lengo
la kupatiwa huduma za jamii zikiwemo afya,elimu,maji pamoja na
miundombinu ambavyo kwa sasa hawajawahi kuvipata huduma hiyo

Mwenyekiti wa Kijiji cha Ngapapa Ngalama Moibo akizungunza na
MTANZANIA alisema kwa sasa huduma walionayo toka wakutanishwe kuishi
Kijijini hapo mwaka 2002 ni kujengewa darasa moja la elimu ya awali na
shirika lisilo la kiserikali la KINNAPA linalofanya kazi ya ushawishi
na utetezi wa masuala ya sera

“Mbali na darasa hilo la kinapa ambalo kwa sasa limechakaa halifai
hata watoto kuingia hapo, tuna matengi ambayo nayo yamechakaa
yaliyokuwa yamejengwa na (WFP) ambao walifika kijijini hapo kuona
maisha ya jamii hiyo ambayo inadaiwa kuishi kwa kula mizizi”

Alisema jamii hiyo wako 300 katika eneo hilo ambapo awali waliahidiwa
kupata huduma za jamii zikiwemo afya,elimu,maji,pamoja na miundombinu
ambayo hawazipati na kuhofiwa kuwa wanaweza kurejea kwenda kuishi
porini kula mizizi kama walivyokuwa wamezoea

Kwa mujibu wa Mkurugenzi mtendaji wa Halamshauri ya wilaya ya Kiteto
Bosco Ndunguru amekiri kuwepo kwa jamii hiyo akidai awali Serikali
iliwataka kuwa pamoja ili waweze kupata huduma za jamii ambazo hadi
sasa wameanza kuzipata kwa kujengewa matenki ya maji pamoja na elimu
mbalimbali za kijamii

Taarifa za uhakika zinasema matenki hayo yalijengwa na Benki ya dunia
ambapo hadi sasa yamechakaa wasione wa kuwasaidia, huku wakiitaka
Serikali kutimiza malengo yao ya kuwasaidia kama walivyoahidi

Jamii ya WANDOROBO imedaiwa kuishi katika mazingira duni na magumu
ambapo kazi ya kuwaunganisha pamoja na kuishi imedaiwa kuwa ngumu huku
jitihada za kutaka kuwasaidia zikitakiwa kuendelea ili wasiweze
kurejea kuishi katika maisha yao ya awali kwa hofu na kutoweka kizazi
hizo ambazo kimedaiwa kupungua kwa kasi kubwa

Mwisho

Maoni