Walemavu na changamoto za kulijenga Taifa MAKALA -1





Mohamed hamad akifanya mahojiano na mzee Kibati wa kibaya juu ya changamoto za walemavu Mkoani Manyara.


Walemavu na changamoto za kulijenga Taifa

MOHAMED HAMAD.
WALEMAVU ni kundi maalumu lililopo ndani ya jamii, kundi hili limesahaulika hali inayotishia ustawi wa maisha yao kutokana na kukosa mahitaji mbalimbali ya kuwezesha waishi ama kuchangia maendeleo yao na Taifa

Kila mtu ana haki na wajibu katika nchi yake kuchangia maendeleo bila kujali jinsia yake kwa hali na mali, lakini katika kada hii inahitaji msaada mkubwa kutoka kwa wadau mbalimbali ikiwemo serikali ili kuwezesha kufanikisha malengo yao

Walemavu wamegawanyika katika makundi mbalimbali, yakiwemo wasioona, wenye upungufu wa viungo, walemavu wa ngozi, walemavu wa mtindio wa ubongo, na viziwi ambao kila kundi linatamani kuchangia maendeleo ya Taifa lao

Katika michango hiyo wengi wao wanashindwa kuchangia kutokana na aina ya ulemavu walio nao, hivyo kuomba msaada kwa wadau na hasa Serikali ili waweze kufikia ndoto zao ambazo zinazidi kufifia siku hadi siku

Makala hii inajikita kuona ushiriki wa walemavu katika uchaguzi na changamoto zinazowakabili kwa zoezi hilo ambalo ni muhimu katika mustakabali wa nchi katika kuchagua na kuchaguliwa

Akizungumzia nafasi ya walemavu kuchangia maendeleo Bw. Ramadhani Athumani Konki mlemavu wa kutosikia wilayani Kiteto alisema, walemavu wanashindwa kushiriki kuchangia shughuli za maendeleo kwa kutokuwa na elimu ya ushiriki kwenye maendeleo hayo

“Walemavu wanahitaji kupatiwa elimu ya utambuzi na mawasiliano ya lugha za alama ili waweze kushiki na jamii vyema katika masuala ya kijamii ambayo yanawezesha Taifa kusonga mbele”alisema Konki

Alisema mbali na changamoto hizo pia wamekuwa wakibaguliwa kwa misingi ya hali walizonazo kwa kuonekana kuwa hawawezi kuchangia maendeleo ndani ya jamii na Taifa kwa ujumla jambo ambalo wanaona kuwa hawatendewi haki

Alisema walemavu wanashindwa kushiriki kikamilifu katika vyombo vya maamuzi kama vikao na makongamano yanayoshushirikisha umma katika maendeleo yao kutokana na mtazamo hasi wa jamii pamoja na mifumo duni ya mawasiliano yaliyopo kati yao na wadau hao

“Huwezi kuomba nyadhifa mbalimbali za uongozi ndani ya jamii, kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo ubaguzi na unyanyapaa, kutokana na aina ya ulemavu tulionao sisi walemavu”alisema

Alisema kumekuwepo na ushiriki hafifu wa walemavu katika hatua mbalimbali za uchaguzi zikiwemo mikutano ya kampeni hali inayofanya wakose haki zikiwemo kuchagua na kuchaguliwa

“Mlemavu wa macho anahitaji kushikwa mkono kwenda kwenye mkutano, halikadhalika viziwi anahitaji kutafsiriwa kinachozungumzwa, kukosekana kwa vifaa vya mawasiliano kumechangia tuwe nyuma kwa kila jambo”alisema Konki

Pia huduma hiyo ikikosekana mlemavu hawezi kuendana na mtu mwengine asiye na ulemavu anayeomba nafasi ya uongozi kwa kufanya ushindani kwa namna yoyote ile ni lazima mlemavu atakosa nafasi kutokana na hali yake, alisisitiza Konki

“Awali tuliona tafsiri ya lugha za alama kwenye baadhi ya vyombo vya habari kama vile TV ingawa wengi wetu hatukuwa na uelewa wa mawasiliano hayo kwa kutokuwa na elimu ya ufahamu wa lugha hiyo lakini ilisaidia, sasa hivi hakuna tafsiri inayotolewa kwa walemavu kwenye vyombo hivyo”

Naiomba Serikali kusaidia kukata mirija ya ubaguzi na kuwezesha upatikanaji wa elimu ya lugha ya alama kwa walemavu ili kuongeza wigo wa walemavu kushiriki maendeleo kwa ujumla, alisema Konki huku akionyesha kukasirishwa kwa kukosa huduma hiyo

Kassimu Ismail Kibati mlemavu wa masikio na kuona alisema, tatizo la Serikali ni kukosekana kwa mfumo imara wa kuwawezesha walemavu kushiriki katika maendeleo ya jamii japo kutoa mapendekezo ya namna ya kusaidiwa “Huwezi kuwazungumzia walemavu wakati huwaoni”alisema

“Ukiangalia hata miundombinu ya majengo ya umma sio rafiki kwa walemavu mfanoss walemavu wa viungo, hali tunayohisi kuwa huo ni ubaguzi wa wazi na ambao unatenga kundi hili ili wasiweze kunufaika na fursa mbalimbali”alisema Kibati

“Kuna mifano hai ya maeneo yetu , tuna viongozi wanaosimamia wasichokiamini kuna  miradi mingi ya ujenzi wa majengo ya umma hakuna miundombinu rafiki kwa walemavu kuingia wakiwa huru kwenda kwa watawala wao na badala yake wanalazimika kupata usaidizi kuwafikia watawala”

Mmoja wa waalimu wa shule ya msingi Kibaya ambaye hakutaka kutaja majina yake gazetini alisema, kuna idadi kubwa ya watoto wenye mahitaji maalumu ambao hawajaandikishwa shule kutokana na Serikali kutokuwa na dhamira ya dhati kusaidia kundi hilo kwa kuanzisha shule maalumu

“Huwezi amini hapa shuleni  tuna wanafunzi 10 tu ambao ni viziwi lakini kuna walemavu ambao hawajaanzishiwa kitengo kama vile wasio ona na wenye mtindio wa ubongo ambao wazazi wamekata tamaa kuwa watoto hao hawawezi kusoma tena””alisema mwalimu huyo

Alisema pamoja na kugundua hili niliweza kuzungumza na wadau mbalimbali wa elimu lakini walishindwa kuchukua hatua kutokana na suala hilo kuwa linahitaji ufadhili mkubwa wa kupata waalimu,vyumba vya madarasa na vifaa vya kujifunzia na kufundishia

Mwisho

Maoni