SERIKALI MBULU YATAMBUA MCHANGO WA MASHIRIKA

Serikali Wilayani Mbulu imesema, inatambua mchango unaotolewa na wadau wa maendeleo zikiwemo taasisi za kidini.

Mkuu wa wilaya ya Mbulu, Chelestino Mofuga, akizungumza kwenye mahafali ya saba ya chuo cha ualimu Waama kilichopo kata ya Bargish alisema, Serikali inatambua michango ya mashirika katika kuihudumia jamii.

Akiongea na wahitimu wa daraja A, wageni waalikwa na jumuiya ya chuo, Mkuu huyo  wa Wilaya alipongeza uongozi wa kanisa la KKKT kwa ushirikiano na serikali, wanapotoa huduma za jamii zikiwemo afya, na elimu.

Alitilea mfano hospitali ya Haydom ya rufaa ya kanda na chuo cha taaśisi ya afya kwamba wamekuwa msaada na kumpongeza Askofu wa kanisa hilo kuwa wanaongeza nguvu katika juhudi za serikali kuwahudumia wananchi.

Kuhusu wahitimu wa cheti cha ualimu amewaasa kusoma hadi chuo kikuu, akitoa mfano wa prof mmoja katika chuo kikuu cha sokoine ambaye alianza na cheti na hakubahatika kupita sekondari lakini leo ni proffesa.

Aliwaasa viongozi hao wa kanisa kuwa na maono ya kusoma alama za nyakati katika awamu ya tano ya Dkt john pombe Magufuli kuwa shule zimeboreshwa  kiasi kwamba zimekuwa ni tishio la kuua shule za binafsi kwani wazazi wengi wanapeleka watoto shule za serikali kutokana na kuwa na imani nazo.

Katika hatua hiyo aliwataka viongozi wa  kanisa kuona mbali na kujifunza soko la wahitimu wao ,kwani kuendelea kutoa mafunzo ya cheti kwa sasa ni sawa na kujiandaa kufunga chuo hicho akidai, serikali imeanza kuäjiri walimu wa shahada ya vyuo kwenda kufundisha shule za msingi na chekechea.

Pia alihoji wahitimu kuwa wanatarajia kupata kazi wapi, kwa ngazi ya cheti akidai inatakiwa kuwa kozi za msingi kuendelea na masomo ,hivyo amewataka kubadili mtazamo na kufikiria kuanzisha chuo kikuu katika wilaya mbulu, ambacho kitatoa kozi mbalimbali zikiwemo za cheti .

Mkuu huyo wa wilaya alisisitiza kuwa mkoa wa Manyara hauna chuo kikuu hivyo waanze kufikiria Wilaya ya Mbulu ili iwe ya kwanza kuanzisha chuo kikuu akisema ni wilaya kongwe ambayo ilianza mwaka mmoja na mji wa Nairobi 1905  lakini haifanani na historia hiyo akisema wanapaswa kukimbia wakati wenzetu wanatembea.

Maoni