Wadau wa Kilimo Kiteto Wapatiwa Elimu Kuhusu Kiwavijeshi  Vamizi

Wadau wa Kilimo Kiteto Wapatiwa Elimu Kuhusu Kiwavijeshi  Vamizi

Wadau wa kilimo wilayani Kiteto wamepata  mafunzo kuhusu kisumbufu kipya cha mimea ya mahindi kinachofahamika kwa jina la  Kiwavijeshi vamizi (Fall Army Worm)

Mafunzo haya yamefanyika  katika ukumbi wa halmashauri ya wilaya ya Kiteto, ambapo washiriki ni wadau wa kilimo kutoka katika makundi mbalimbali 

Wamo wakulima, wauzaji wa pembejeo za kilimo, maafisa ugani, waheshimiwa madiwani, viongozi wa dini na  mheshimiwa mkuu wa wilaya ambaye amewakilishwa na kaimu katibu tawala (W) ndugu Musa Waziri.

lengo la mafunzo hayo  ni kujenga uelewa wa pamoja kwa wakulima dhidi ya kiwavi jeshi vamizi.

Wataalamu wa kilimo kutoka wizara ya Kilimo kwa kushirikiana na Shirika la Chakula na Kilimo Duniani ( FAO) waliwasilisha mada tatu ambazo ni  utambuzi , uchunguzi na ufuatiliaji pamoja na udhibiti wa viwavijeshi vamizi.

Akiwasilisha mada ya kwanza ambayo ni utambuzi , Afisa kilimo ndugu Sergea Mutahiwa  ameelekeza kuhusu namna ya kumtambua kiwavijeshi vamizi ,mzunguko wa maisha yake, tabia zake,muonekano wake.

Pia ameeleza kuhusu hali ya viwavi jeshi nchini, ushirikishwaji wadau, usambazaji wa machapisho, ushiriki wa vyombo vya habari na mtazamo wa jamii kuhusu viwavijeshi vamizi .

Akizungumzia mtazamo wa jamii, ndugu  Mutahiwa amesema kwamba kwa sababu ya uelewa mdogo  wa viuatilifu vinavyopendekezwa na jinsi ya kuvitumia,

Wakulima wameendelea  kutumia viatilifu  vingi vya aina mbalimbali,  na katika maeneo mengine wakulima hutumia dozi kubwa kutokana na mashambulizi kujirudia .

Mutahiwa amesisitiza kwamba  matumizi  yasiyo sahihi ya  viatilifu yanaweza kusababisha  kuua wadudu wasiolengwa  na  kudhuru afya za binadamu ,vilevile kusababisha usugu  kwa visumbufu vya mimea.

Aidha ameelekeza  viatilifu vinavyoshauriwa na  Taasisi ya Utafiti wa Viuatilifu (TPRI)  sambamba na hayo ameeleza hatua za baadae ambazo serikali kupitia wizara ya kilimo inatarajia kuzichukua ili  kudhibiti kisumbufu hicho.

Mada ya pili ni  ukaguzi na ufuatiliaji, mada hii  imetolewa na bibi Grace David ambapo ameelekeza  jinsi ya kufuatilia ukuaji wa mimea shambani, kwamba mimea inatakiwa kufuatiliwa katika ukuaji wake

Ufuatiliaji utawezesha  kubaini uwepo na mwenendo wa visumbufu vya mimea  katika eneo husika.

Vilevile ameelekeza namna ya kufanya ukaguzi,  kwamba ukaguzi ufanyike zigizaga, usifuate mstari  ili kuwakilisha shamba zima  na usichukue zaidi ya dakika 15 .

Aidha Grace David amesisitiza kwamba ukaguzi ni muhimu ili kubaini  uwepo na kiasi cha viwavijeshi vamizi, na kufanya tathmini ya madhara ili kuweza kujua njia sahihi ya kufanya udhibiti.

Kadhalika ameelekeza jinsi ya kutumia mtego maalum wenye harufu kwa ajili ya kukamata viwavijeshi vamizi.

Mada ya tatu ni udhibiti wa viwavi jeshi vamizi,mada hii imetolewa na ndugu Ayubu  Nchimbi , ambapo  ameelekeza kwamba udhibiti wa kiwavijeshi vamizi unaanza na utambuzi,

Ilielezwa kuwa lazima kumtambua kisumbufu,mzunguko wa maisha yake , dalili za mashambulizi, na kiasi gani mashambulizi yamefanyika.

Na kwamba dalili za  mashambulizi ndizo zitakazomuongoza mkulima  kujua kiasi cha mashambulizi, na njia atakazotumia ili kudhibiti kisumbufu.

Vilevile Nchimbi amesema kwamba udhibiti sahihi wa viwavijeshi vamizi  katika ukuaji wa mimea ya mahindi unategemea na muda wa utambuzi wa mashambulizi ya mdudu kupitia ufuatiliaji na ukaguzi wa mimea shambani.

Ndugu Nchimbi ameelekeza kuhusu hatua za ukuaji wa mahindi, amesema  kwamba ukuaji wa mahindi uko katika sehemu mbili; ya kwanza ni  kujiimarisha kwa mmea, na ya pili ni uzaaji wa mmea.

Na kwamba ufuatiliaji ni muhimu ili kuweza kudhibiti visumbufu mapema kabla mashambulizi hayajawa makubwa.

Akizungumza kwa niaba ya mkuu wa wilaya ya Kiteto kaimu katibu tawala wa wilaya ndugu Musa Waziri amewataka washiriki wa semina hiyo kupeleka elimu waliyoipata katika maeneo wanayoishi.

“Mkienda kukaa kimya bila kuelimisha wengine, hiki kilichofanyika leo kitakuwa hakina maana, na mtakuwa hamkuitendea haki wizara ya kilimo pamoja na hawa wataalamu  wake waliofanya kazi kubwa ya kutupatia elimu hii.

Kila mmoja aliyeshiriki semina hii ahakikishe anatoa elimu hii kwa watu zaidi ya kumi”.

Aidha Waziri amesema kwamba, kwa kuwa  mkuu wa wilaya huwa anafanya mikutano mingi vijijini kila watakapokuwa katika mkutano, atahakikisha kwamba anatoa elimu ambayo ameipata katika semina hiyo.

Naye afisa Kilimo wa wilaya ndugu Robert Urassa amewashukuru washiriki wa semina  kwa kuhudhuria na amewaomba ushirikiano, ili kwa pamoja waweze kuwaelimisha wakulima kama ambavyo wamepata elimu katika semina hiyo.

Katika hatua nyingine diwani wa kata ya Bwagamoyo mheshimiwa Yahya Masumbuko amesema kwamba semina hiyo imewajengea uelewa wa kutosha kuhusu kiwavijeshi vamizi.Sambamba na kauli hiyo Mhe.

Masumbuko ametoa rai kwa wizara ya Kilimo kwamba semina hizo zisiishie tu katika ngazi  ya wilaya,bali zifike hadi vijijini kwani  ndiko waliko wakulima wengi zaidi.

Semina hiyo imehitimishwa  kwa washiriki pamoja na wawezeshaji kwenda katika shamba lililopo jirani na ofisi za TRA  Kiteto ambapo wameweza kujifunza kwa vitendo jinsi ambavyo kiwavijeshi vamizi anavyofanya mashambulizi katika mimea ya mahindi, na kumuona kiwavijeshi vamizi katika hatua zote kama ambavyo wameelekezwa katika semina

Wataalamu wametoa maelezo  ya kina kuhusiana na kiwavi huyo,pamoja na kujibu maswali yote ambayo yaliyokuwa yakiulizwa na washiriki ambao wamekuwa na shauku kubwa ya kufahamu zaidi baada ya kujengewa uelewa.

Maoni